UTANGULIZI
Nawapa hongera wanakijiji kwa kuamsha mijadala mizito namna hii, lakini naona bado hatujafikia mwafaka wa namna gani tutekeleze suala hili, ili mawe hayo yatokomee kwa kumezwa na mimea. Najua mwafaka utapatikana tu hapa hapa kijijini, kwani sisi wanakijiji tunatofautiana mitazamo na tuna ujuzi wa namna anuwai, haya yote ni katika kufanikisha malengo haya.
HOJA
1. UMILIKI BINAFSI
Kimsingi naunga mkono wachangiaji wanaosema kuwa hakuna mtu anayeyajua vyema, nje ndani mazingira ya hapo Ilula kwenye mawe kama wenyeji wenyewe wa mahali hapo. Hii iwe ndio hoja ya msingi kabisa katika kutafuta utatuzi wa janga hili la uharibifu wa mazingira, na iwe ndio chanzo cha kutafuta ufumbuzi, sio wa eneo hilo la Ilula tu, lakini hata kwa maeneo mengine ambayo yameathiriwa kama hilo. Naamini ufumbuzi utapatikana kwa kuwashirikisha hao hao wenyeji wa mahali hapo, kama wachangiaji walivyofafanua hapo juu. Kwamba, waliokata miti kwa ajili ya kuni, mbao, ujenzi, uchomaji wa mkaa na kadhalika huenda hawakutoka mbali na hapo, kwa hiyo ni hao hao. Kwa hiyo basi, naunga mkono hoja ya wao kushirikishwa katika kuhuisha mimea ya eneo husika. Hali kadhalika naunga mkono hoja za wachangiaji wenzangu, kuwa eneo husika liwe chini ya umiliki binafsi, tuache habari ya mali ya umma (Tragedy of the Commons), kwani haina uchungu. Watu wakimilikishwa maeneo haya watayaheshimu na watachukua hatua kwa wale wanaoyaharibu. Mfano mwingine wa mbinu shirikishi, kwa kujazia kwa Analyst ni mradi wa CAMPFIRE, ulio nchini Zimbabwe. Unaweza kusoma zaidi habari zake kwa kufuata kiungo hiki "http://www.resourceafrica.org/documents/1993/1993_campfire_bg.pdf".
2. TUSICHANGANYE SIASA NA UTAALAMU
Nimuunge mkono mwanakijiji anayeponda suala la kampeni za zimamoto za kupanda miti (potiticizing technical problems). Nami nashindilia misumari katika jeneza la kuzikia kampeni hizi za zimamoto. Kwa uzoefu wa nchini mwetu,mahali pengi katika nchi yetu kampeni hizi za zimamoto zimefeli, kwani watu wengi hujiandaa kwa siku hiyo tu, kampeni ikishapita na suala linasahaulika. Tusitarajie mbio za mwenge ama siku ya mazingira duaniani kutatua tatizo hili, hizi ni siasa, kamwe hazitengamani na hali halisi ya tatizo. Analyst na Makafoo nadhani wamefafanua vya kutosha tatizo hili. Kwamba tupande miti kwa sababu mwenge unapita ama ni siku maalumu hata kama hali hairuhusu, ni uendawazimu. Suala hili linahitaji utatuzi wa kitaalamu na sio siasa, na kama nilivyosema, wataalamu wa mwanzo kabisa ni hao wenyeji wa maeneo hayo yaliyoathiriwa. Baadaye sasa, mbinu za utaalamu za kisasa zichanganywe na uzoefu wa wenyeji hawa ili kuleta matokeo bora. Pia nichukue nafasi hii kupinga suala la kuanza kukurupushana na serikali kuu ama za mitaa wakati huu, kwani tutarudi kule kule, kama mwenzangu mmoja alivyochangia, kuweka vikao ili katika vikao hivi tujadili mahali kwa kwenda kufanyia vikao vya kutatua tatizo hili bila kuwashirikisha wakaazi wa eneo husika.
3. MLISHONYUMA
Kwa sababu wataalamu wa kwanza na wa kuaminika kwa mtazamo wangu ni wanakijiji wa eneo husika, naamini wao ndio wanaojua ni miti ama mimea ya namna gani ilikuwa inastawi katika eneo husika. Kwa hiyo basi, iwapo wazo ni kurejesha mimea katika eneo husika, sio vibaya kama ile mimea ya mwanzo (original indigeneous species)ikapewa kipaumbele,ndipo mimea mingine (exotic species)ipewe nafasi. Inawezekana mimea ya mwanzo isikubali katika eneo husika kulingana na ukubwa wa athari, lakini pia mimea vamizi ina athari zake, na huenda isistawi vyema. Inabidi tuwe makini na hili, kwani tusije kurudi kule kule, leo tunapanda mikaratusi, kesho tunaambiwa tukate kwa kuwa inaharibu vyanzo vya maji. Aibu!
4. MCHANGANYIKO WA MBINU
Kwamba tunapanda miti ili kutokomeza mawe ya pale Ilula isiwe ndio hitimisho la janga hili. Inabidi tuwasaidie wanakijiji wa eneo husika kuwa na majiko sanifu yanayotumia kuni kidogo sana, ili hata kama watakata miti hapo baadaye kwa ajili ya kuni basi kasi ya ukataji iwe ndogo kuliko urejeshaji. Suala la kukata miti kwa ajili ya kuni halikwepeki kwa mazingira kama ya Ilula, na kwa Tanzania inayofanana na Ilula, najua kuna baadhi watapinga, lakini kabla ya kupinga tujiulize, ni wangapi tunatumia majiko ya umeme majumbani kwetu? Ni wangapi tuna uhakika kuwa umeme leo hautakatika kabisa? Je bei ya mafuta ya taa ikoje? Je huyu mwanakiji anatumia jiko la mchina kama wewe wa mjini? Je anaweza kununua mkaa kama wewe?
5. MCHANGO WA HALI NA MALI
Ilula ni eneo moja tu kati ya maeneo anuwai ya nchi yetu yaliyokumbana na athari za uharibifu wa mazingira. Sema bahati nzuri kwamba lipo njiani na hivyo limepigwa picha kiasi kwamba tumeliona. Na kama ilivyo ada, Mtanzania anaruhusiwa kuishi popote pale ndani ya Jamhuri yetu, kwa hiyo basi huwezi kujua lini na wewe siku moja utajikuta upo Ilula, ama lini hapo kwako pakawa dampo lenye athari mbaya zaidi ya hizi tunazojadili. Kwa maana hii suala la kusaidia eneo husika ni la sisi wanakijiji hiki pamoja na wengine wote, kwa kishirikiana na wanakijiji wa Ilula. Wamiliki wa Ilula ni sisi sote! Tujitoe kwa kila hali na mali kufanikisha suala hili. Niko tayari kutoa mchango wa hali na mali tukimaliza mjadala huu. Bw Mjengwa kaweka mawasiliano hapa kijijini, nitawasiliana nae!
HITIMISHO
Ndugu wanakijiji wenzangu, kama kamera iliyotumika kupiga picha hii ya mawe ya Ilula ilinunuliwa kwa michango ya wanakijiji, kwa nini isiwezekane kubadili eneo hilo pichani na mengine yaliyoathirika kama hilo kwa jina la kijiji hiki? Jamani, hii ndio kazi ya kijiji hiki, kuikomboa Tanzania kwa namna yoyote ile. Kwamba, mwisho wa mjadala huu iwe ni mwanzo wa utekelezaji wa mawazo haya ya wanakijiji.
Wananakiji wenzangu naomba kuwasilisha!
http://jadili.blogspot.com
Mkataba wa Buzwagi ulisainiwa nje haraka ili kukwepa gharama
Habari Zinazoshabihiana
� Udurusu mikataba ya madini wakamilika 15.08.2007 [Soma]
� Suala la rada danadana tupu 08.02.2007 [Soma]
� Kikwete asifia mradi wa Buzwagi 24.08.2007 [Soma]
*Barrick yasema majadiliano yalichukua muda mrefu
*Yasema kisheria mkataba unaweza kusainiwa popote
*Yaeleza jinsi uchumi wa nchi utakavyokua kwa kasi
Na Said Mwishehe
KAMPUNI ya uchimbaji Madini ya Barrick Gold Tanzania imesema mkataba wa mgodi wa Buzwagi uliharakishwa kusainiwa Uingereza ili kuepuka upandaji gharama za uendeshaji.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa Barrick Gold Tanzania, Bw. Deo Mwanyika, kutokana na majadiliano juu ya kusainiwa kwa mkataba huo kuchukua muda mrefu, Barrick iliiomba Wizara ya Nishati na Madini kuharakisha uamuzi wake kwa vile ucheleweshwaji wa utiwaji saini ulikuwa ukiuathiri vibaya.
"Tuliona ni vema tukaharakisha utiaji saini wa mkataba huo baada ya kuona kwamba kama tutachelewa kuna hatari za kuathirika kwa mradi wenyewe kutokana na kupanda kwa gharama za vifaa kila kukicha. Kwa mfano kati ya Juni mwaka jana na Januari mwaka huu, gharama za mradi ziliongezeka kwa kiasi cha dola milioni 20 za Marekani," alisema.
Kwa upande wa Barrick alisema kulikuwa na ulazima wa kuharakishwa utiaji saini huo kabla ya mwisho wa mwaka huu, ili makao makuu ya kampuni hiyo yaweze kuweka mgodi wa Buzwagi katika mpango wa makadirio ya mwaka.
Bw. Mwanyika alisema kutokana majadiliano yaliyofikiwa kati yao na Wizara ya Nishati na Madini, waliarifiwa kuwa mkataba wa Buzwagi ungekuwa umesainiwa ifikapo Februari 16 mwaka huu.
"Barrick tuliambiwa kwamba vibali vyote kutoka vyombo husika vya Serikali vilikuwa vimepatikana. Kutokana na hali hiyo waliendelea kukamilisha taratibu za kusaini mkataba Februari 16 mwaka huu ikiwa ni pamoja na kuandaa maofisa wake walioidhinishwa kusaini mkataba huo na nyaraka zinazoendana na mamlaka hizo," alisema Bw. Mwanyika.
Hata hivyo, alisema kwa bahati mbaya, ilipofika Februari 15 mwaka huu, wakaambiwa kwamba mkataba huo usingeweza kusainiwa kutokana na Waziri wa Nishati na Madini kuwa katika ziara ya Rais Jakaya Kikwete katika nchi za Ulaya.
"Kutokana na kuona kwamba kuna hatari ya kutosaini mkataba huo wakati muda unazidi kwenda, uongozi wa Barrick uliwasiliana na Wizara na kupendekeza kwamba isingekuwa vema kuahirisha utiaji saini mkataba huo, kwa vile taratibu zote za maandalizi zilishakamilika," alisema Bw. Mwanyika.
Alisema baada ya kutoa ombi hilo, ndipo walipoarifiwa na Wizara kwamba Bw. Karamagi angepatikana London, hivyo ujumbe wa Barrick uliondoka Tanzania na kwenda Uingereza ambapo mkataba ulisainiwa Februari 17 mwaka huu katika Hoteli ya Churchil ambapo mbali na maofisa wengine wa Wizara ya Nishati kuwapo, pia Balozi wa Tanzania nchini London, Bibi Mwanaidi Maajar naye alikuwapo.
"Ni kweli tulisaini hotelini na hilo si kosa, kwani mkataba unaweza kusainiwa mahala popote pale, ilimradi uzingatie sheria na taratibu. Kuhusu nani alichukua mhuri na nyara nyingine za Serikali, hadi Uingereza hatujui, ila inawezekana ni maofisa waliokuwa Tanzania ambao tulikuwa tukijadiliana nao juu ya suala hilo nchini na baadhi yao tulikuwa nao wakati wa utiaji saini, hivyo inawezekana ndio waliokwenda na nyaraka hizo za Serikali," alisema.
Hata hivyo alisema Barrick haina ofisi wala kampuni Uingereza na wao pia walikuwa wageni ambao walikwenda huko kwa jukumu la kuhakikisha mkataba unasainiwa kama ilivyokuwa imepangwa na kukubalina na Serikali. Lakini ni vema mambo mengine muwaulize maofisa wa Wizara ya Nishati na Madini," alisema.
Akieleza zaidi juu ya mgodi wa Buzwagi, Bw. Mwanyika alisema pamoja na kusaini mkataba, bado kwa sasa mgodi huo hauna faida kutokana na kwamba hauna dhahabu ya kutosha, ambayo inalingana na gharama zitakazotumika kujenga mgodi huo.
Alisema mradi wa machimbo ya Buzwagi ni mgodi mdogo unaohitaji uwekezaji mkubwa wa dola milioni 400.
"Mradi wa Buzwagi ni mdogo, kwa sababu pamoja na kutumia dola milioni 400 ili kuuchimba, utazalisha wakia milioni 2.4 ikilinganishwa na mgodi wa Bulyanhulu ambao ulitumia dola milioni 280 kutoa wakia milioni 10 za dhahabu," alisema Bw. Mwanyika.
Alisema kutokana na kukosekana kwa dhahabu ya kutosha katika mgodi huo, hakuna kampuni ya uchimbaji duniani ambayo ingekubali kusaini mkataba wa uchimbaji madini ambao utaleta faida ya sh. bilioni 800 kutokana na makato ya kodi mbalimbali kwa kipindi cha miaka 10.
Alisema mbali na Serikali kupata kiasi hicho cha fedha, pia wanakijiji wa Mwima ambao ndio wako katika eneo la mgodi wa Buzwagi, wamelipwa fidia sh. milioni 78 mbali na sh. milioni 60 zitakazokuwa zikitolewa kila mwaka kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya wana kijiji.
Vilevile wakati wa ujenzi wa mgodi huo, uchumi wa Tanzania utaongezeka, kwani wakati wa ujenzi kiasi cha sh. bilioni 450 zitapatikana na wakati wa uzalishaji, sh. trilioni 1.3 zitapatikana katika kipindi chote.
"Kusainiwa kwa mgodi wa Buzwagi, nchi itapiga hatua kiuchumi, kwani wananchi watafaidika na mgodi huo kutokana na ajira zitakazopatikana, lakini pia ni kuhakikisha maendeleo ya wananchi yanaboreshwa hasa walioko eneo husika," alisema Bw. Mwanyika.
Alisema ajira mpya zaidi ya 900 zitatokana na uwekezaji huo katika kipindi cyha ujenzi na kuingiza jumla ya sh. bilioni 75 kama mishahara.
"Vile vile kutakuwapo na ajira nyingine 700 zitakazoingiza jumla ya sh. bilioni 130 wakati wa uendeshaji wa mgodi," alisema Bw. Mwanyika.
Mgodi wa Buzwagi umeingia katika duru za habari baada ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Bw. Zitto Kabwe, kuwasilisha hoja bungeni akidai kuwa kitendo cha kusaini mkataba wa mgodi huo nje ya nchi kilikuwa na dosari.
Bw. Kabwe kutokana na hoja yake, alitaka iundwe Kamati Teule ya Bunge kuchunguza mazingira ya mkataba huo akidai kuwa Waziri wa Nishati na Madini, Bw. Karamagi, alikuwa amelidanganya Bunge. Hata hivyo mambo yalimgeuka na kujikuta akisimamishwa kazi hadi Januari mwakani