Mazingira yanatisha. Mtoto aliyeshika tairi anakua akiizoea hali ya uchafu huu. Nyuma yake kuna watoto wenzake wanaocheza karibu na mfereji wa maji machafu. Nyuma kushoto kuna kijiwe cha vijana. Hawana ajira. Katika mazingira haya kipindupindu na malaria vitaendelea kuua watoto wetu na hata watu wazima. Hivi hizi pesa za MKUKUTA zinatumika vipi? Na wasomi wetu wanaijua hali hii halisi. Kwanini tunafumbia macho?


Maggid,
Nimeiangalia picha hii kwa takribani dakika kumi nzima bila kupekua kope.Nimeitolea macho namna hiyo sio kwa sababu siamini bali imenikumbusha hali halisi ya mazingira mengi nchini Tanzania,sio Mwananyamala peke yake.
Pamoja na hayo swali moja la msingi sana sina budi kujiuliza,hivi ni jukumu la nani kusafisha mazingira? Katika nchi kama hii ninayoishi ni jukumu la serikali za mitaa,jiji nk.Lakini tofauti moja kubwa hapa ni kwamba serikali hizi za mitaa,jiji nk zinawezeshwa na kodi za wananchi.Hali najua ni tofauti nchini mwetu.Utaratibu wa kulipa kodi bado haupo na sababu ni kwamba wananchi hawaamini katika kazi ya kodi zaidi ya kwenda kujaza matumbo ya "waheshimiwa".Sasa basi hapo nadhani jukumu la kusafisha mazingira yetu linarudi kwa mwananchi mwenyewe.Sikubaliani na kisingizio cha umasikini kama matokeo ya uchafu uliokithiri namna hii.Unaweza kuwa na nguo iliyochoka lakini hiyo sio sababu ya kutoifua na kuipiga pasi.
Kinachotokea hapa ni kwamba viongozi wa mitaa,wale wajumbe na mabalozi wa nyumba kumi kumi(hivi bado wapo?) hawajui kazi zao.Mabwana na mabibi afya wa huko wanatakiwa kufukuzwa kazi mara moja.Pia umuhimu wa kujitolea haupo kabisa inaonekana! Kwanini?