Precision Air yazindua safari ya Mwanza - Nairobi
Jumapili, Julai 5, 2009:
SHIRIKA la ndege la Precision Air limezindua safari ya moja kwa moja ya kutoka Mwanza, Tanzania kwenda Nairobi, Kenya.
Uzinduzi huo uliofanyika mwishoni mwa wiki jijini Mwanza, unafanya Precision Air kuwa na safari za moja kwa moja 13 katika huduma zinazotolewa na shirika hilo Afrika Mashariki, na safari 381 zinazofanywa na ndege za shirika hilo kwa wiki, hivyo kuzidi kupanuka kwa mtandao wake Tanzania.
Katika kuzindua safari hiyo, baadhi ya abiria na wadau wa Precision Air, walisafiri kutoka Nairobi na kutua Mwanza walikolakiwa na baadhi ya maofisa wa Precision Air, wakiwamo Meneja wa Precision Air Kanda ya Ziwa, Cecilia Odemba, Ofisa Mawasiliano wa Precision Air, Mabhe Matinyi na Ofisa wa Ratiba na Mipango ya Mtandao wa Precision Air, Patrick Mwakasungula.
Pia wasafiri hao wakiwamo waandishi wa habari na wadau wengine wa sekta ya usafiri wa anga, walilakiwa na Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Leonard Bihondo kabla ya kutembelea maeneo mbalimbali ya Jiji la Mwanza.
Safari hiyo kati ya Nairobi na Mwanza, kwa kiasi kikubwa itarahisisha usafiri kati ya miji hiyo na itafupisha muda wa safari kuwa saa 1 na dakika 20 tu ikilinganishwa na saa 2 na dakika 45 iwapo ndege itapitia Kilimanjaro.
Safari hizo za moja kwa moja kutoka Mwanza kwenda Nairobi na kutoka Nairobi kwenda Mwanza, zitakuwa zikifanyika mara nane kwa wiki. Awali, shirika hilo la ndege Ð ambalo asilimia 49 inamilikiwa na Shirika la Ndege la Kenya (Kenya Airways) Ð lilikuwa likifanya safari mara nne kwa wiki kutoka Mwanza kupitia Kilimanjaro.
ÒSafari ya moja kwa moja kwenda Mwanza itawarahisishia abiria usafiri. Pia itaboresha usafiri wa kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) kwenda Afrika Kusini, Dubai, London, Entebbe na Doha,Ó alisema Alfonce Kioko, Mkurugenzi Mkuu wa Precision Air.
Alisema shirika hilo limewekeza katika safari hiyo ya Mwanza ili kuwarahisishia wateja usafiri na kuwalenga zaidi wafanyabiashara wa samaki na bidhaa nyinginezo jijini Mwanza.
Kioko alisema abiria wengi katika njia hiyo ni wasafiri kati ya Mwanza na Nairobi na pia kuna abiria wengine wanaohitaji kwenda JKIA ili kuunganisha ndege nyingine.
ÒIdadi ya abiria wanaosafiri na ndege za Precision Air imeongezeka kutoka 216,990 kwa mwaka 2004 hadi 538,305 mwaka huu,Ó alisema Kioko.
Precision Air hivi sasa inafanya safari zake katika mikoa 13 nchini na ina mpango wa kupanua wigo kwa kufanya safari za kimataifa katika miji ya Luanda, Lubumbashi, Johannesburg, Harare, Pemba na Nampula, Msumbiji, Lilongwe na Hahaya, ikiwa ni sehemu ya kujiimarisha zaidi.
Pia, katika kuboresha safari za ndani ya nchi, Precision Air inatarajia kuanzisha safari katika miji ya Mbeya, Songea, Dodoma, Pemba Zanzibar na Tanga.

























